Loan

1.0        MAELEKEZO MUHIMU KWA WAOMBAJI WAPYA

Uongozi wa Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu Zanzibar unapenda kuwajulisha waombaji wote wa Mikopo ya Elimu ya Juu kwa mwaka wa masomo 2021/22 kuwa maombi yao wanapaswa kuyawasilisha kupita mfumo malum wa maombi ya mtandaoni unaojulikana  ZHELB Online Loans Application System (ZOLAS).

Mtandao huu umeunganishwa na mitandao ya Tasisisi nyengine za Elimu ya Juu, Fedha na vitambulisho zikiwemo Tume ya Taifa ya Vyuo Vikuu (TCU), Baraza la Mafunzo ya Ufundi (NACTE), Baraza la Taifa la Mitihani (NECTA) na Mamlaka ya Usajli wa Matukio Maalum ya Kijamii ya Zanzibar (ZCSRA) inayotoa vitambulisho vya Mzanzibari Mkaazi. Mwombaji hatohitajika kujaza taarifa zinazopatikana katika taasisi.

Aidha, ZOLAS imeunganishwa na mfumo maalum wa malipo na ujumbe mfupi wa maneno (sms) kupitia mitandao ya simu.

Waombaji wote wanafahamishwa kuzingatia mambo yafuatayo:

i.      Kuwa na kitambulisho cha Mzanzibari.

ii.     Kuhakikisha kuwa nambari ya mtihani wa kidato cha nne iwe sawa na nambari aliyoituma kuwasilisha maombi ya kujiunga na chuo.

iii.   Kuhakikisha kuwa majina yake matatu yanayotumika kwenye kitambulisho cha Mzanzibari na kidato cha nne yanalingana.

iv.   Wahitimu wa nje ya Tanzania wawe na ithibati ya ulinganisho (Equivalence) kutoka NECTA kwa kidato cha nne na sita, NACTE kwa Stashahada na TCU kwa Shahada.

v.    Wahitimu wa Stashahada wawe na Award Verification Number (AVN) kutoka NACTE).

vi.   Kuwa na baruapepe (email) binafsi na ambayo haitobadilika kwa wakati wote wa mchakato wa maombi.

vii.  Kuwa na nambari ya simu iliyosajiliwa.

viii.Kuhakikisha kufanya malipo stahiki ya maombi kwenye akaunti ya BMEJZ baada ya kufungua akaunti na kupatiwa nambari ya kumbukumbu (control number) ya kufanyia malipo hayo.

ix.   Kurudufu (scanning) nyaraka zote muhimu zinazohitajika wakati wa maombi zikiwemo barua za kukubaliwa kujiunga na masomo, matokeo (transcript) na vyeti vya kumalizia masomo kwa waombaji shahada ya uzamili na shahada ya uzamivu. Waombaji wote wa vyuo vya nje ya nchi mbali ya kuwa na barua za kujiunga na chuo wanapaswa pia kuambatisha barua kutoka Tume ya Taifa ya Vyuo Vikuu zinazoridhia kujiunga na Chuo na kusoma fani husika.

x.    Maombi ya mikopo yanapaswa kuwa na taarifa sahihi.

2.0        JINSI YA KUTUMA MAOMBI

Waombaji watume maombi kwa njia ya mtandao kupitia tovuti ya BMEJZ (https://zhelb.go.tz) na kubonyeza kitufe cha Online Loan Application System. Aidha, waombaji wanaweza kutuma maombi yao kupitia kiunganishi zolas.zhelb.go.tz/zolas.

Ili kuweza kuwasilisha maombi hayo, kila mwombaji anatakiwa kukamilisha hatua zifuatazo:

2.1        Kujisajili

Baada ya kubofya kiunganishi zolas.zhelb.go.tz/zolas utafunguka ukarasa ambao mwombaji atapaswa kujaza nambari ya Kitambulisho cha Mzanzibar Mkaazi na nambari ya mtihani wa kidato cha nne.

Angalizo:

·       Majina matatu ya muombaji yanayotumika kwenye kitambulisho cha Mzanzibari na kidato cha nne yanalingana. Vyenginevyo utashindwa kusajiliwa na kuendelea na hatua nyengine zinazofuata.

·       Nambari ya mtihani wa kidato cha nne iwe sawa na nambari iliyotumika kuwasilisha maombi ya kujiunga na chuo

Baada ya kukamilika kwa hatua hii, mwombaji ataingiza nambari yake ya simu ya mkononi, anuani ya baruapepe na nambari ya mtihani wa kidato cha sita akiwa ni mhitimu wa kidato cha sita au nambari maalum ya utambulisho (Award Verfication Number – AVN) kwa mhitimu wa Stashahada.

2.2        Kufungua akaunti (ZHELB Online Student Account)

Baada ya mwombaji kukamilisha kujisajili, mfumo wa ZOLAS utamtumia nambari maalum (Code) kwenye anuani ya baruapepe aliyowasilisha. Mwombaji ataingia tena katika mfumo wa ZOLAS na kufungua akaunti ambayo jina la mtumiaji (username) itakuwa na nambari yake ya Kitambulisho cha Mzanzibari Mkaazi na neno la siri (password) atatumia nambari maalum aliyotumiwa. Baada ya kufungua akaunti, mwombaji anapaswa kubadilisha nambari maalum aliyotumiwa kwa kuingiza neno jipya la siri kulingana na chaguo lake.

2.3        Kutuma maombi

Ufunguzi wa akaunti unamwezesha mwombaji kutuma maombi kwa kufuata maelekezo yaliyopo na kujaza kikamilifu kila kipengele husika ikiwa ni pamoja na waombaji wa mikopo kulipa TZS 20,000 ambazo ni gharama za maombi zinazolipwa kupitia mitandao ya simu ya mkononi. Malipo yatafanyika baada ya mwombaji kupatiwa nambari maalum (control number). Malipo yatakayofanyika bila ya kutumia nambari maalum hayatozingatiwa.

Kwa maelezo zaidi tembelea zolas.zhelb.go.tz/zolas.

3.0        SIFA ZA WAOMBAJI

3.1        SIFA ZA KUPATA MIKOPO

Sifa za waombaji wa mikopo ambao maombi yao yanaweza kuzingatiwa wakati wa uteuzi zimetajwa kwenye kifungu cha 20 cha Sheria Na. 3/2011 ya BMEJZ.

Sifa hizo ni zifuatazo:

a)    Awe Mzanzibari mwenye kitambulisho cha Mzanzibari Mkaazi.

b)    Awe amewasilisha maombi yake kupitia mfumo wa mtandao wa maombi wa BMEJZ ndani ya muda maalum uliowekwa.

c)    Awe amepata alama nzuri za ufaulu zinazomruhusu kupata udahili kwenye chuo cha elimu ya juu kinachotambuliwa na mamlaka husika nchini

i.            Mwombaji wa shahada ya kwanza (Bachelor/First Degree) aliyehitimu kidato cha sita anapaswa awe amefaulu angalau masomo mawili (Principal subjects) kwa alama za ufaulu zinazoanzia 4.0. Mwombaji aliyehitimu Stashahada anatakiwa kuwa na alama za ufaulu (GPA) zinazoanzia 3.0.

ii.           Mwombaji wa shahada ya uzamili (Master/Second Degree) au shahada ya uzamivu (Doctor of Philosophy - PhD) awe na ufaulu kuanzia daraja la pili.

iii.          Mwombaji mpya anayeendelea na masomo anaweza kuomba kwa kuzingatia sifa za kitaaluma zilizotajwa hapo juu [c(i) –(ii)]. Aidha muombaji awe amefaulu mitihani yake ya chuo kwa kiwango kitakachomwezesha kuendelea na masomo kwa mwaka unaofuatia katika ngazi ya masomo anayoombea mkopo.

d)    Awe ameomba fani inayolingana na vipaumbele vya Taifa (Angalia Kiambatisho Na. 1).

e)    Asiwe na mkopo au udhamini wa masomo kutoka taasisi nyengine.

f)     Ukomo wa umri wakati wa kutuma maombi usiozidi miaka 35 kwa Mwombaji wa shahada ya kwanza, miaka 45 kwa mwombaji wa shahada ya uzamili na miaka 47 kwa mwombaji wa shahada ya uzamivu.

g)    Mwombaji anayedaiwa na BMEJZ awe ameshaanza kulipa deni lake kwa angalau asilimia 25 ya deni lote bila ya kusita kwa malipo ya deni ya kila mwezi. Ikumbukwe kuwa malipo ya asilimia 25 ya mkopo wa awali siyo dhamana ya kupangiwa mkopo.

h)    Mwombaji aliyesoma kwa mkopo kutoka BMEJZ awe ameshafanya kazi kwa angalau miaka miwili baada ya kuhitimu masomo yake ya awali kabla ya kuomba mkopo mwengine kutoka BMEJZ.

i)     Waombaji wa vyuo vya nje wapate ithibati ya kukubaliwa kujiunga na chuo (No Objection Certificate) kutoka Tume ya Vyuo Vikuu ya Tanzania.

Wanafunzi wanaoendelea na masomo ambao ni wanufaika wa mikopo hawahitajiki kuwasilisha maombi mapya ya mikopo. Wanafunzi hao wanapaswa kujaza mikataba kwa kila mwaka mpya wa masomo unapoanza pamoja na kuwasilisha matokeo ya mitihani.

4.0        UTEUZI WA WAOMBAJI

4.1        KUTANGAZWA WAJINA YA WAOMBAJI WALIOTEULIWA

Orodha za majina ya waombaji walioteuliwa kwa kila chuo na fani yatatangazwa kupitia tovuti za BMEJZ na WEMA katika mwezi wa Oktoba 2021. Aidha, kila mwombaji atakayeteuliwa atatumiwa taarifa ya uteuzi kupitia baruapepe na ujumbe mfupi wa simu.

4.2        KUJAZA MIKATABA

Mkataba ni hati ya makubaliano kati ya BMEJZ na mwanafunzi ambapo BMEJZ itampatia muombaji mafao stahiki baada ya muombaji huyo kutimiza masharti yote yaliyoainishwa kwenye Mkataba.

4.2.1   MIKATABA YA WAOMBAJI WAPYA

Waombaji wapya wa mikopo na ufadhili wa masomo wa SMZ watapaswa kujaza mikataba ili kuweza kunufaika na mafao yanayotolewa na BMEJZ. Ili kuweza kujaza mkataba, mwombaji aliyeteuliwa atapaswa kuingia kwenye akaunti yake aliyoitumia wakati wa kuwasilisha maombi ya mikopo au ufadhili wa masomo wa SMZ.

Kupitia akaunti hiyo, mwombaji atapatiwa nambari maalum ya kumbukumbu ya kufanya malipo (Control Number) kabla ya kuendelea na hatua nyengine za kujaza mikataba.

4.2.2   MIKATABA YA WANUFAIKA WANAOENDELA NA MASOMO

Wanufaika wa mikopo na ufadhili wa masomo wa SMZ wanaoendelea na masomo mwaka 2021/22 katika Taasisi mbalimbali za Elimu ya Juu za ndani na nje ya nchi ambao hawakutuma maombi yao kwa njia ya mtandao, wataendelea kujaza mikataba inayopatikana katika ofisi za BMEJZ za Unguja na Pemba.

Wanafunzi waliojaza mikataba yao ya awali kwa njia ya mtandao, watapaswa kujaza mikataba mipya kwa kuhuisha taarifa zao kulingana na mwaka wa masomo uliopo.

5.0        MAFAO KWA WAOMBAJI WA MIKOPO

5.1        VIPENGELE VYA MAFAO

Kwa kuzingatia uhitaji wa waombaji wa mikopo na ufadhili wa masomo wa SMZ, BMEJZ inalipa gharama za masomo kwa baadhi ya mafao kama ifuatavyo:

Na.

Mafao kwa waombaji wa mikopo vyuo vya ndani

Mafao kwa waombaji wa mikopo wa vyuo vya nje

1.

Ada ya masomo na mitihani

Ada ya masomo na mitihani

2.

Posho la chakula na malazi

Posho la chakula na malazi

3.

-

Tiketi ya ndege

4.

-

Bima ya afya

 

5.2        UTARATIBU WA MALIPO

Posho la chakula na malazi, gharama za vitabu na viandikwa na gharama za mafunzo kwa vitendo zitalipwa moja kwa moja kwenye akaunti ya benki ya mwanafunzi. Ada ya masomo na mitihani na mahitaji maalum ya kitivo yatalipwa moja kwa moja kwenye Taasisi husika.

6.0        WAOMBAJI WA MIKOPO NJE YA NCHI

Kwa mwaka 2021/22, waombaji wa masomo katika Taasisi za Elimu ya Juu za nje ya nchi watakaoteuliwa kupata mikopo ni wale amabao fani za masomo yao ni za Vipaumbele vya Taifa na hazifundishwi katika Taasisi za Elimu ya Juu za Tanzania hasa katika kada maalum za afya, uhandisi, mafuta na gesi, kilimo, uvuvi na tiba za mifugo.

Waombaji wapya wa mikopo wanaotarajia kujiunga au wanaoendelea na masomo katika taasisi za elimu ya juu nje ya Tanzania, wanapaswa kuchagua ama kulipwa ada ya masomo au posho la kujkimu pekee. Hakuna mwanafunzi atakayelipiwa ada ya masomo na posho la kujikimu kwa pamoja.

Aidha, malipo ya ada yamewekwa ukomo maalum unaolingana na US$ 3,200 kwa mwaka na tofauti ya ada itakayojitokeza italipwa na mwafunzi husika. Utaratibu huu unatekelezwa ili kumjengea mnufaika wa mikopo ya BMEJZ mazingira wezeshi ya kurejesha deni lake bila ya usumbufu baada ya kuhitimu masomo yake.